Wednesday, August 14, 2013

Simba yaikimbia 3 Pillars,yachomoa kucheza dakika za mwisho

Mabingwa wa zamani wa Tanzania wekundu wa Msimbazi Simba wamechomoa kucheza na 3 Pillars ya Nigeria,mchezo uliokuwa uchezwe leo Uwanja wa Taifa.

Wakati maandalizi yote yakiwa yamekamilika na Simba kukubali kucheza mchezo huo wa kirafiki,viongozi wa klabu hiyo wamebadilika dakika za mwisho baada ya kutokea kutoelewana baina yao wenyewe viongozi wa klabu hiyo.


Katika kikao walichokaa August 6 kuzungumzia mchezo huo na waandaji walioileta timu ya 3 Pillars,Simba waliwakilishwa na katibu mkuu wake Evodius Mtawala na wakakubali kucheza mchezo huo ambao mpaka leo asubuhi walikuwa wakisisitiza kucheza lakini wakabadili maamuzi kufikia mchana leo.

Juhudi za mwenyekiti wa klabu hiyo Ismail Aden Rage kuona mchezo huo unafanyika ziligonga mwamba baada ya mjumbe mmoja wa kamati ya utendaji kuwashinikiza wenzake mchezo huo usichezwe nao wakakubaliana naye.

Imeshuhudiwa mabasi yakiendelea kushusha mashabiki waliokwenda uwanjani kushuhudia mnyama akiserebuka na 3 Pillars lakini wamekutana na hali tofauti.

Kaimu Makamu mwenyekiti wa Simba Joseph Itangáre akizungumza na mratibu wa mchezo huo Jerry Kotto amesema sababu kubwa kwao ni kuogopa kuharibu heshima yao waliyoiweka mbele ya SC Villa ya Uganda waliyoigonga mabao 4-1 kwenye tamasha la Simba day Wikiendi iliyopita.


No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.