Saturday, August 17, 2013

Nadir Canavarro na bahati yake Yanga

Nahodha mpya wa Yanga Africa Nadir Haroub Ally Canavarro ameanza kukitumikia cheo chake cha unahodha na bahati ya kunyanyua taji lake la kwanza.

Canavarro ambaye hapo kabla alikuwa nahodha msaidizi wa klabu hiyo amechukua mikoba ya unahodha kutoka kwa Shadrack Nsajigwa aliyemaliza mkataba na sasa amegeukia kazi ya ukocha akiifundisha Lipuli ya Iringa.

Tokea amekabidhiwa cheo hicho hilo ni taji lake la kwanza kupokea,wakilipata baada ya kuwashinda Waoka mikate wa Azam FC kwa bao 1-0 lililofungwa na Salum Telela kwenye mchezo wa ngao ya jamii uliochezwa uwanja wa Taifa Dar Es Salaam.

Katika mchezo huo uliochezwa uwanja wa Taifa umeshuhudia wachezaji wa zamani wa Simba beki Kelvin Yondan na kipa Ally Mustapha Barthez wakishindwa kuendelea na mchezo katika dakika 20 za kwanza za kipindi cha kwanza baada ya kuumia na kushindwa kurudi uwanjani.

Nafasi ya Yondan ilichukuliwa na Mbuyu Twite wakati nafasi ya Barthez ikachukuliwa na kipa mpya aliyetokea Azam Deogratius Munishi Dida.

Mchezo huo wa ngao ya jamii umefungua msimu mpya wa ligi kuu ya Tanzania bara unaoanza kuunguruma wikiendi ijayo ya August 24 na Yanga watafungua pazia kwa kucheza na Ashanti United watoto wa Ilala waliorejea kwa mara nyingine katika ligi kuu.

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.