Monday, June 30, 2014

Suarez amuangukia Chiellin,aendelea kujikanyaga kwenye utetezi wake

Mshambuliaji wa Liverpool Luis Suarez amemuomba radhi mchezaji wa Italia aliyemng'ata Giorgio Chiellini na kusababishwa kupigwa adhabu ya kufungiwa mechi tisa za kimataifa na kifungo cha miezi minne kutojihusisha kwa namna yoyote na mchezo wa soka.

Suarez mwenye miaka 27 amesema ukweli ni kuwa Chiellini alipata maumivu ya kung'atwa baada ya kugongana.

Kauli hiyo inaendelea kujichanganya baada ya awali kusema kuwa alikosa balance na hakumng'ata Chiellini.

Hii ni mara ya tatu kwa Suarez kuhusika na tukio la kung'ata,itakumbukwa aliwahi kumng'ata beki wa Chelsea Branislav Ivanovic April 2013 akiwa kwenye timu yake ya Liverpool na pia amewahi kumng'ata Otman Bakkal wakati alipokuwa akiitumikia Ajax mwaka 2010.

Suarez anajutia kitendo hicho alichomfanyia Chiellini na kuomba radhi kwa mchezaji huyo na familia ya mpira na kuahidi kuwa hatarudia tena kufanya kitendo kama hicho.

Chiellini mwenyewe amemtumia ujumbe Suarez kwenye mtandao wa kijamii wa Twitter, akimwambia yote yamesamehewa na anaamini FIFA watampunguzia adhabu.

Suarez atakosa mechi 9 za kwanza za ligi kuu ya England na anarejea katika soka October 26.


Rais Mujica wa Uruguay aitusi FIFA kisa Suarez


Rais wa Uruguay Jose Mujica amewatukana maafisa wa FIFA kwa kuwaita ''kundi la watoto wa Mbwa''.

Hatua hiyo inafuatia maafisa wa shirikisho hilo kumshushia rungu Luis Suarez akifungiwa mechi tisa za kimataifa na kupigwa marufuku kujihusisha na mchezo wa soka kwa miezi minne baada ya kupatikana na hatia ya kumng’ata mchezaji wa Italia Georgio Chiellin.

Rais huyo wa Uruguay anayesifika kwa kutotafuna maneno na kutumia matamshi makali ameiita adhabu hiyo kama adhabu ya kinazi.

Aliyatoa matamshi hayo kupitia televishini ya taifa alipokuwa anawapokea wachezaji wa timu hiyo baada ya kusukumwa nje ya fainali za kombe la dunia.

Rais huyo alifunika mdomo wake kwa mshutuko wa kile alichosema , lakini waandishi wa habari tayari walikuwa wamemrekodi.

Rais Mujica amesema FIFA ilimuadhibu Suarez kwa sababu ya maisha yake ya zamani ambayo yalikuwa ya unyonge na akaitaja adhabu hiyo kama aibu kubwa kwa historia ya FIFA.

Kocha Algeria akerwa na swali la kuhusu wachezaji wanaofunga mfungo wa Ramadhan


Kocha wa timu ya taifa ya Algeria ambayo inashiriki kombe la dunia nchini Brazil, Vahid Halilhodzic amekataa kuweka wazi idadi ya wachezaji wake ambao wanafunga mfungo wa Ramadhan kabla ya mechi yake na Ujerumani inayopigwa leo.

Mfungo huo ambao ni wa siku 30 ulioanza jana Jumapili umemfanya kocha Halilhodzic, mwenye umri wa miaka 61, kukataa kujibu swali kama wachezaji wake watafunga Ramadhan au la wakati wakicheza fainali hizo za kombe la dunia.

Kocha huyo amesema hilo ni swala binafasi na anapoulizwa yeye ni kukosa nidhamu na heshima kwakuwa katika hilo kila mchezaji atafanya anavyotaka.

Mfungo wa Ramadhan ni sharti kwa kila muisilamu na ni moja ya nguzo za imani ya dini ya kiisilamu, ingawa wagonjwa na wazee wanaruhusiwa kutofunga.

Watu ambao wanasafiri au kwenda vitani pia wanaruhusiwa kutofunga ambalo pia linawea kuangukia kwa wanamichezo.

Kocha huyo amesema kuwa si mara ya kwanza kuwa na wachezaji waisilamu katika timu anayofundisha huku akisema yeye mwenyewe ni Muisilamu lakini hawezi kumlazimisha mtu kufuata anachotaka yeye katika dini na huwaacha huru wachezaji kuamua wanachotaka.

Nyota wa timu hiyo Madjid Bougherra, amesema anafunga kama kawaida ingawa mchezaji wa Ujerumani Mesut Ozil na mchezaji wa Ufaransa Bacary Sagna ambao ni waisilamu wamesema hawatafunga.

UDANGANYIFU : Roben akiri kujiangusha kudai penati


Mshambulizi wa Uholanzi Arjen Robben amekiri kuwa alidanganya na kujirusha ili timu yake ipate penalti japo anakiri hakufanyiwa madhambi na nahodha wa Mexico Rafael Marquez.

Roben ameomba radhi mashabiki kwa kudanganya na kujiangusha,akikiri wazi kuwa ilikuwa njia ya kutaka kuisaidia timu yake.

Kocha wa Mexico Miguel Herrera amemponda mwamuzi wa mechi yao na Uholanzi Pedro Proenca kwa kuipendelea Uholanzi .

Herrera amesema kuwa Penalti hiyo ya dakika tatu kabla ya kukamilika kwa mechi hiyo haikupaswa kutolewa na hiyo akiiona ni njama ya FIFA kuiondoa Mexico kwenye fainali hizo.

Herrera amesema haikuwa sahihi kwa mwamuzi kutoka Ulaya kuchezesha mchezo kati ya timu kutoka Ulaya dhidi ya timu kutoka Marekani ya kusini.

Anauliza kwanini FIFA hawakupanga mwamuzi kutoka Africa,Asia au kutoka Marekani Kusini.

Robben alikuwa akiingia kwenye lango la Mexico na kujiangusha kumdanganya mwamuzi na kusababisha penati ambayo ilitumbukizwa na Jan-Klaas Huntelaar iliyoipa tiketi ya kutinga robo fainali timu yake ya Uholanzi.