Monday, September 30, 2013

UTATA : Torres akabiliwa na kifungo cha mechi 4

Mshambuliaji wa Chelsea Fernando Torres anaweza kukabiliwa na adhabu ya kukosa michezo minne kufuatia kadi nyekundu aliyooneshwa wikiendi iliyopita huko White Hart Lane kwenye mchezo dhidi ya Tottenham.

Tayari kocha wa The Blues Jose Mourinho amemtupia lawama Jan Vertonghen kwa kudanganya mwamuzi Mike Dean kitendo kilichomfanya kumuonesha Torres kadi ya pili ya njano na kufuatiwa na kadi nyekundu.
 

Lakini Torres sasa anakabiliwa na shtaka la kumshika usoni Vertonghen katika picha zinazomuonesha mkono wa Torres ukimshika usoni mchezaji huyo licha ya video kuonesha hakuna tatizo lolote kwa tukio hilo lililomfanya kutolewa nje lakini Torres hana haki ya kukata rufaa kwa mujibu wa kanuni za FA.

Anakabiliwa na makosa ya kinidhamu na atakuwa mchezaji wa kwanza kuhukumiwa na jopo jipya la kamati ya ligi na FA la kupitia video.

Mwamuzi Mike Dean anatakiwa kutolea ufafanuzi kuhusu kadi ya kwanza ya njano ambayo alimpa Torres.
 

Inaonesha kuwa Torres alipewa kadi ya njano kwa tukio la kwanza baada ya filimbi kupigwa na si kwa tukio la pili la mshambiliaji huyo kumshika usoni Vertonghen,tukio ambalo tayari Dean anakiri kuwa hakuliona.

Hiyo inalipeleka suala hilo kwenye kamati hiyo ya kupitia video ambayo inaundwa na waamuzi wa zamani na kama itabainika kosa hilo ni la vurugu,Torres ataongezewa mechi tatu za ziada ambazo jumla itakuwa mechi nne.
 
Kama atakumbwa na adhabu hiyo Torres atakosa mechi dhidi ya Cardiff na Manchester City na pia atakosa mchezo wa Capital One Cup dhidi ya Arsenal,na baadaye mchezo dhidi ya Norwich.

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.