Wednesday, November 13, 2013

Ramires aigomea Real Madrid,aipa tano Chelsea,Mourinho


KIUNGO wa Chelsea Ramires amesema hana mpango wa kuondoka Stamford Bridge licha ya kuwepo kwa habari za chini chini kuwa atatolewa kwenda Real Madrid katika mpango wa kubadilishana na Sami Khedira.

Kiungo huyo raia wa Brazil amekuwa anawindwa na wakali hao wa Hispania ikonekana chaguo sahihi la kuziba nafasi ya Khedira ambaye ameshaweka wazi nia yake ya kutaka kuondoka Santiago Bernabeu.

Chelsea ni moja ya klabu zinazovutiwa na Khedira iwapo Madrid watakubali kumuuza na kuna habari za chini chini kuwa inawezekana klabu hizo zikabadilishana viungo hao.

Lakini Ramires,ambaye amesaini mkataba wa miaka mitano wa kuendelea kuwepo Chelsea mpaka 2017 mwaka uliopita amekuwa ni mchezaji muhimu akipata nafasi ya kucheza chini ya kocha mpya Jose Mourinho.

Ramires anasema anatambua kazi yake nzuri barani Ulaya ndio inayowafanya Real Madrid kuhitaji huduma yake lakini bado ana mkataba na Chelsea na kwake ni kwenda kinyume na maadili kusema lolote na linabaki kuwa habari zisizo na uhakika.

Anasema ana furaha ya kuendelea kuwepo kwenye klabu yake hiyo ambako pia anaheshimika akiwa sehemu ya historia na kama ataondoka, Chelsea ndio watafanya maamuzi.

Anazidi kufunguka kuwa kwake anatambua kuwa Chelsea ni moja ya klabu kubwa duniani na anataka kuendelea kucheza mpira na kuisaidia timu yake kupata mataji.

Ramires akamwagia sifa Mourinho akisema ni kocha mwenye heshima,anayefanya kazi nzuri,akiwahamasisha wachezaji na kutoa nafasi kwa kila mmoja.

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.