Monday, December 23, 2013

BREAKING NEWS : Yanga wamtimua kocha Brandts

Timu ya Yanga imetangaza rasmi kumtimua kocha wake mkuu raia wa Uholanzi Ernie Brandts ikiwa ni siku chache baada ya kula kibano cha mabao 3-1 kutoka kwa mahasimu wao Wekundu wa Msimbazi Simba kwenye mchezo wa hisani wa Nani Mtani Jembe.

Akitangaza maamuzi magumu yaliyofikiwa na kamati ya utendaji Mwenyekiti wa kamati ya mashindano ya klabu hiyo ambaye pia ni mwenyekiti wa kamati ya usajili Abdallah Binkleb amesema wamefikia uamuzi wa kumtimua kazi Brandts kwakuwa tayari uwezo wake ulifikia mwisho.

Yanga walimuongeza mkataba kocha huyo hivi karibuni na wameamua kuuvunja kwa kutoridhishwa na kiwango kinachooneshwa na timu hiyo licha ya kufanya usajili wa kuboresha kikosi.

Brandts anaondoka kwenye klabu hiyo huku akiwa amewapa ubingwa wa ligi kuu msimu uliopita na akiiacha timu hiyo ikiongoza ligi mpaka mzunguko wa kwanza unamalizika.

Kocha msaidizi Fred Felix Minziro na kocha wa makipa Razak Siwa wao wanaendelea kubakia katika timu hiyo.

Itakumbukwa Brandts alitua Yanga akitokea APR ya Rwanda msimu mmoja nyuma.

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.