Friday, April 4, 2014

EXCLUSIVE : Kaseja kuigomea Yanga hii ndio sababu


Sasa imebainika sababu ya golikipa wa Yanga Juma Kaseja kugoma kuingia kambini kujiandaa na mchezo wa ligi kuu dhidi ya JKT Ruvu kabla ya baadaye kukubali kujiunga na wenzake kambini huko Bagamoyo.

Baada ya mazoezi ya hapo juzi jioni yaliyofanyika viwanja vya Tanganyika Packers Kawe Kaseja aliwafuata viongozi wa benchi la ufundi Kocha Van Der Pluijm,msaidizi wake Boniface Mkwasa na kocha wa makipa Juma Pondamali akiweka msimamo wa kutoingia kambini kutokana na tuhuma hizo anazoshushiwa.

Kaseja aliwaambia wazi kuwa hawezi tena kudaka katika mechi zinazofuata kwakuwa haamini tena ndani ya kikosi hicho.

Sababu kubwa ya Kaseja kugoma kuingia kambini na kuichezea klabu hiyo ni ujumbe mfupi wa vitisho katika simu yake ya mkononi aliokuwa anatumiwa na mashabiki na wanachama wa klabu hiyo pamoja na simu alizokuwa akipigiwa wakitaka awaachie timu yao kinyume chake atakumbana na balaa atakalolijutia.

Ujumbe huo mfupi na simu hizo zilikuwa zikimtuhumu waziwazi kuwahujumu kwa kufungisha katika mechi za ligi kuu ili waukose ubingwa uende kwa Azam FC wanaoongoza ligi.

Simu ya kipa huyo wa zamani wa Simba na Moro United ilikuwa bize kupokea simu na ujumbe mfupi ambao ulikuwa wa vitisho na ndipo alipoona haina sababu ya kuendelea kuitumikia klabu hiyo.

Hata hivyo baadhi ya viongozi wa Yanga walikaa naye katika kikao na kumshawishi aingie kambini na aendelee kuitumikia klabu hiyo kwakuwa wao ndio viongozi na wanamuhitaji katika timu na vizuri akasikiliza kutoka kwao kama viongozi na si mtu mwingine.

"Unajua tulikaa naye Kaseja tukazungumza na tukamueleza hali halisi ya hicho kinachotokea na tumemwambia kuwa sisi ndio viongozi na ndio tunamuhitaji kwahiyo hana sababu ya kusikiliza mtu mwingine wa nje"alisema mtoa habari ambaye alisisitiza kutotajwa jina kwakuwa yeye sio msemaji wa klabu.

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.