Monday, January 27, 2014

Sakata la Owino Logarusic bado tata


Huko kwa Wekundu wa Msimbazi Simba licha ya kupata ushindi wa bao 1-0 dhidi ya Rhino Rangers kwenye mchezo wa ligi kuu hapo jana,hali ya mambo si shwari baada ya kocha wake Zdravko Logarusic kugomea beki Joseph Owino kujumishwa kikosini.

Suala hilo la Owino linaonekana kuwavuruga baada ya kutibuana na Loga mazoezini na kwenye mchezo wa jana hakuwepo kabisa kikosini.

Suala hilo pia limeonekana kuwagawa viongozi wa Simba ambao bado wanaona Owino ana umuhimu mkubwa kwenye kikosi hicho hasa sehemu ya ulinzi.

MJUMBE KAMATI YA UTENDAJI
Mmoja wa wajumbe wa kamati ya utendaji aliyezungumza na supermariotz kwa masharti ya kutotajwa jina amesema wazi kuwa kocha huyo huenda akaondoka Simba mapema zaidi kwasababu ya msimamo aliouweka kwenye suala hilo.

"Unajua tulijaribu kumuombe msamaha Owino baada ya kutibuana na kocha mazoezini lakini kocha ameonesha msimamo anasema tuchague Owino awe nje ya timu yeye abaki ndani au yeye aondoke na Owino arudi kwenye timu sasa hili linatuweka njia panda,japo tunatambua mchango wa Owino na tunamuhitaji"Alisema mnyetishaji huyo kutoka kamati ya utendaji.

Amesema inawezekana kocha huyo akawa na muda mfupi wa kukaa Simba hasa kwasababu ya tabia zake za kuwatukana wachezaji mazoezini kama ilivyotokea kwa Owino na kutokubali ushauri.

MATOLA ABANWA
Kocha msaidizi wa Simba Suleima Matola akabanwa kuhusu suala la Owino akasema hawezi kuzungumza suala hilo kwa upana kwakuwa liko juu ya uwezo wake lakini anachojua ni kwamba Owino alitofautiana na kocha Logarusic kwenye mazoezi na ndio sababu ya kutokuwepo kambini wakati wakifanya maandalizi kwenye mchezo wa jana dhidi ya Rhino Rangers.

WANACHAMA WAKATIA NENO
Wanachama wa klabu hiyo nao baada ya mechi dhidi ya Rhino Rangers kwenye mkusanyiko wa vikundi kila mmoja alikuwa akisema lake kuhusiana na Owino na kocha Logarusic.

Wengine wamemuunga mkono Loga wakisema ni kocha anayekomesha nidhamu mbovu kwenye kikosi huku wengine wakiwa tofauti wakisema anakosea kuwatukana wachezaji na kuwagombeza kama watoto wadogo jambo ambalo sio sawa.

Lakini pia wengine wakawa wanamlalamikia kwa kitendo cha kumuingiza na kumtoa baada ya dakika 12 mshambuliaji Betram Mwombeki aliyechukua nafasi ya Hamis Tambwe na yeye nafasi yake ikachukuliwa na Henry Joseph Shindika.

UONGOZI
Uongozi wa Simba chini ya mwenyekiti wake Ismail Aden Rage unaendelea kushughulikia mzozo huo wa Owino na Loga ili kupata utatuzi wa kuinufaisha timu hiyo kwa mzunguko wa pili wa ligi kuu ambao bado Simba wapo kwenye nafasi ya nne.

No comments:

Post a Comment

Note: Only a member of this blog may post a comment.